1.0 UTANGULIZI
Hi! Karibu kwenye darasa letu fupi la Usalama Wa Vipodozi Vyako ambapo leo tutaangazia vipodozi visivyo salama na madhara yake. Mimi ninayekuletea mada hii naitwa Said, mtaalam wa dawa ambaye ninajishughulisha na dawa za binadamu na vipodozi kila siku. Kama utakuwa na tatizo sehemu au swali basi karibu sana uniuize nami nitakujibu au nitakushauri au kukupa msaada mwingine tofauti kadiri itakavyohitajika.
Vipodozi visivyo salama ni vipodozi ambavyo vina kemikali zinadhuru au zinazoweza kuudhuru mwili na kuusababishia matatizo. Maana hii inaweza kuongezewa na kujumuisha vipodozi vyote ambavyo usalama wake unatia mashaka na vinaweza kuleta madhara kwa mtumiaji.
Hivyo hujumuisha :
-Vipodozi ambavyo havijasajiliwa na mamlaka ya serikali (TBS kwa Tanzania Bara au ZFDA Kwa Zanzibar)
-Vipodozi vyenye viambata (kemikali) vya sumu na vilivyopigwa marufuku na mamlaka ya serikali (TBS kwa Tanzania Bara au ZFDA Kwa Zanzibar)
-Vipodozi ambavyo muda wake wa matumizi umeisha
-Vipodozi ambavyo havioneshi tarehe ya kuharibika (mwisho wa matumizi)
-Vipodozi ambavyo maelezo yake hayajaandikwa kwa Kiswahili au kiingereza
Vinaweza vikawa ni mafuta, losheni, krimu, pafyumu, poda na kadhalika.
1.1 VIAMBATA (KEMIKALI) VYA SUMU VILIVYOPIGWA MARUFUKU
Vingi vikiwa katika lugha ya kiingereza, hizi ndizo kemikali ambazo huongezewa katika vipodozi ili kufanikisha au kusaidia dhumuni lililolengwa kwa kipodozi husika. Viambato vyenye sumu vilivyopigwa marufuku ni:
1. Chloroquinone (Hydroquinone na kemikali zingine)
2. Steroids (Mifano ni Betamethasone, Beclomethasone, Hydrocortisone, Clobetasol, na Dexamethasone)
3. Mercury (Zebaki) na kemikali zinazotokana nayo
4. Chloroform
5. Bithionol
6. Hexachlorophene
7. Mercury (Zebaki) na kemikali zinazotokana nayo
8. Vinyl chloride
9. Zirconium na kemikali zinazotokana nayo
10. Methyelene chloride
11. Halogenated salicylanilides (Dimetabromsalan, Trimetabromsalan na Tetrabromsalan)
12. Chlorofluorocarbons (Kwenye pafyumu na deodorants)
1.2 JINSI YA KUJUA KAMA KIPODOZI KINA KIAMBATO (KEMIKALI) CHA SUMU KILICHOPIGWA MARUFUKU
Angalia kwenye lebo ya kipodozi chako sehemu waliyoandika Ingredients au Contents au neno jingine lolote lenye maana ya Vitu vilivyomo ndani. Hapo angalia kama kuna kiamabato au kemikali yoyote ambayo nimeiandika hapo juu kuanzia namba 1 mpaka 12.
Kama kuna kiambato au kemikali ambayo imepigwa marufuku basi jua kipodozi chako sio salama. Acha kukitumia mara moja na toa taarifa kwa mamlaka ya serikali (TBS kwa Tanzania Bara au ZFDA Kwa Zanzibar)
Kama hakuna kiambato cha sumu basi kipodozi chako kinaweza kuwa salama. Tatizo linakuja pale watengenezaji wanapofanya uhuni kwa kudanganya au kuficha na kuacha kuandika baadhi ya viambato vilivyomo ndani. Ambalo pia ni kosa kisheria.
MIFANO :
1. Sabuni ya JARIBU ina kiambato MERCURY. Sabuni hii sio salama, haifai kwa matumizi na imepigwa marufuku.
2. Losheni/krimu ya MEKAKO ina kiambato HYDROQUINONE. Losheni/krimu hizi sio salama, hazifai kwa matumizi na zimepigwa marufuku
3. Krimu za FAIR & LOVELY SUPER CREAM, VISIBLE DIFFERENCE CREAM, SKIN SUCCESS FADE CREAM, DEMOVATE NA DIPROSON CREAM zina viambata STEROIDS. Krimu hizi sio salama kutumika kama vipodozi na zimepigwa marufuku.
Mwisho wa somo la kwanza, fuatilia somo la pili......
Kama una swali au unahitaji ushauri tafadhali wasiliana nasi AFYA ZAIDI (AZ) CONSULTANTS kupitia WhatsApp 0788179686 au Email: afyazaidi@gmail.com au tembelea website yetu: https://afyazaidi.co.tz
Kuna namna nyingine ya kutambua kiambata sumu ikiwa haijaandikwa kwenye lebo?